Walalamika Rais Magufuli kufuta Siku ya Ukimwi dakika za mwisho

Baadhi ya wadau wa Siku ya Ukimwi Duniani wamelalamika kupata hasara kubwa baada ya serikali kuyafuta, huku wakiwa tayari wameshafika m...


Baadhi ya wadau wa Siku ya Ukimwi Duniani wamelalamika kupata hasara kubwa baada ya serikali kuyafuta, huku wakiwa tayari wameshafika mkoani Singida yalikokuwa yafanyike kitaifa.

Wadau hao ambao walikuwa washiriki maonyesho yaliyokuwa yaambatane na maadhimisho hayo, wamedai hatua hiyo ya serikali pia itawasababisha wapate usumbufu na matatizo makubwa wakati wa kurejea makwao, ikiwamo tatizo la nauli kwani baadhi yao wametoka mikoa mbalimbali.

Wakizungumza mjini hapa jana, wadau hao walisema wanapongeza hatua ya Rais Dk. John Magufuli, kufuta maadhimisho hayo, lakini hatua hiyo ingefanyika mapema badala ya kushitukiza hali iliyosawababishia usumbufu mkubwa.

“Hatua ya Rais wetu ni nzuri kwa sababu dawa hospitalini zitapatikana kwa wingi, lakini amaetushitukiza mno, angesema mapema ili tusije kabisa huku Singida,” alisema Singu Hussein Singu, mjasiriamali wa tiba asilia kutoka mkoa wa Kilimanjaro.

Akiunga mkono kauli hiyo, Andrew Venance, mjasiriaamali wa tiba asilia kutoka Dar es Salaam, alisema haelewi atarejeaje nyumbani kutokana na kuishiwa nauli baada ya kutumia fedha nyingi kwa nauli na malazi.

Akizungumzia malalamiko ya washiriki hao, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk. Parseko Kone, alisema hatua hiyo ya Rais Dk. Magufuli itawasaidia wananchi wengi kupata dawa hospitalini, hususani kwa waathirika wa virusi vya ukimwi.

Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani mwaka huu, ilikuwa yaanze Novemba 25 hadi Desemba Mosi, mwaka huu mjini Singida. 

Rais Dk. Magufuli alipangwa  kuwa mgeni rasmi wakati wa ufungaji wa maadhimisho hayo.


Related

Kitaifa 3606878944157618453

Post a Comment

emo-but-icon

item