Chadema Waigaragaza Polisi Mazishi ya Mawazo
Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza imemaliza utata kuhusu kuagwa ama kutoagwa jijini Mwanza kwa mwili wa marehemu Alphonce Mawazo, aliyekuwa ...
http://taarifayahabari360.blogspot.com/2015/11/chadema-waigaragaza-polisi-mazishi-ya.html
Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza
imemaliza utata kuhusu kuagwa ama kutoagwa jijini Mwanza kwa mwili wa marehemu
Alphonce Mawazo, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema) mkoani Geita.
Jaji Lameck Mlacha,
alitoa uamuzi juu ya shauri hilo mahakamani hapo jana, akisema marehemu Mawazo
ana haki ya kikatiba kuagwa na kufanyiwa ibada Mwanza, ambako baba yake mdogo
anaishi.
Uamuzi huo ulitolewa
kutokana na ombi la muombaji ambaye ni baba mdogo wa marehemu, Charles Lugiko
dhidi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza na Mwanasheria Mkuu wa Serikali
kufuatia zuio la mwili huo kuugwa jijini Mwanza.
Hukumu hiyo iliyoanza
kusomwa saa 7:30 mchana na kuhitimishwa saa 8:22 mchana.
Jaji Mlacha alisema baada ya
kupitia maombi ya mapitio ya muombaji (Lugiko) dhidi ya kamanda wa polisi kwa
ajili ya hati ya dharula, ameona kuna kasoro katika zuio hilo.Alisema kifungu
30 (3) cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
kinachozungumzia haki ya
msingi ya raia, kinasema mtu yeyote anayeona haki yake imeingiliwa au kuvunjwa,
anaweza kwenda Mahakama Kuu ili kuweka zuio.
Jaji Mlacha alisema kwa
mujibu wa kifungu cha 19, marehemu ana haki ya kuagwa na ndugu, jamaa, marafiki
na wafuasi wa chama chake na pia kufanyiwa ibada kutokana na imani yao.
Alisema alichofanya kamanda
wa polisi hata wanasheria wa serikali waliomwakilisha walikubaliana mwili huo
kuagwa Mwanza, lakini walichopinga ni namna ya uagaji wake ulivyopangwa. “Mtu
asiangaliwe kwa historia yake ya nyuma, bali kinachotakiwa aangaliwe kwa muda
uliopo sasa…
Mawazo anaangaliwa zaidi
kisiasa kwa ngazi ya kitaifa, pia mlezi wake anaishi Mwanza,” alisema Jaji
Mlacha.
Jaji Mlacha alisema si jambo
geni kwa mtu kufariki sehemu nyingine, kuagwa sehemu nyingine na kuzikwa sehemu
nyingine, hivyo marehemu Mawazo ana haki ya kikatiba kuagwa na kufanyiwa ibada
Mwanza ambako baba yake mdogo anaishi.
Jaji huyo alisema, iwapo
polisi waligundua kutakuwa na vurugu wakati wa uagaji wa mwili huo jijini
Mwanza, wasingetoa amri ya zuio kwani walifanya hivyo wakijua wanaondoa haki
kikatiba. “Kamanda wa polisi ana haki ya kuwaita ndugu na viongozi wa Chadema
na kuzungumza nao na wala si kuwanyima haki yao kikatiba…haki ya kisheria
ilikuwa ni kuwaita wote na kukubaliana,” alisema.
Aidha, Jaji Mlacha alisema
kifungu cha 5 (1) kilichotumiwa na Mwanasheria wa Serikali Mkuu, Seth Mkemwa,
kuwa kamanda wa polisi ana haki hiyo, si kweli kwani kifungu hicho hakimpi mamlaka
polisi kufanya hivyo zaidi ya kulinda amani.
“Hivyo, amri iliyotolewa na
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza si sahihi na Mahakama Kuu inafutilia mbali
mamlaka hiyo ya kamanda,” alisema. Baada ya kutoa hukumu hiyo, Jaji Mlacha
alitoa maelekezo kwa muombaji na viongozi wa Chadema kukutana na kamanda wa
polisi mkoa haraka ili wapange jinsi ya kufanya ibada na kisha kuaga mwili wa
marehemu.
Pia alimtaka kamanda wa
polisi azingatie hukumu hiyo iliyotolewa pamoja na kutakiwa kuweka ulinzi ili
watu waweze kufanya ibada na kuaga pasipokuwapo na silaha nzito.
JAJI AWAONYA CHADEMA
Hata hivyo, aliwataka
viongozi wa Chadema wakati wa shughuli hiyo kujiepusha na kauli zinazoweza
kuchochea hasira za wafuasi wa chama hicho kwani marehemu ameuawa na watu
wasiojulikana.
“Nawaomba viongozi wa
Chadema wajizuie kutoa kauli za kuleta mihemko kwa wafuasi wa chama chao
kutokana na marehemu kuuawa na watu wasiojulikana,” alisema.
chanzo:ippmedia
