Mkapa Amsifu Kikwete kwa UDOM

Raisi Mstaafu Mhe, Kikwete alipotemebelea Kituo cha Sayansi UDOM RAIS mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa amepongeza jitihada za...

Raisi Mstaafu Mhe, Kikwete alipotemebelea Kituo cha Sayansi UDOM

RAIS mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa amepongeza jitihada za Rais wa Awamu ya Nne Jakaya Kikwete kwa kutekeleza kwa vitendo dhana iliyokuwepo ya ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM).

Mkapa, ambaye ni Mkuu wa Chuo hicho alisema dhana ya ujenzi wa chuo hicho ilikuwepo tangu awamu ya uongozi wake lakini mara alipoingia madarakani Rais mstaafu Kikwete akaitekeleza, jambo ambalo ni la kupongezwa.

Aidha aliwaasa wahitimu wa vyuo vya elimu ya juu hapa nchini kutumia taaluma zao kujiajiri ili elimu yao itumike kuwanufaisha Watanzania wote kwa maslahi ya taifa huku akijivunia mafanikio yaliyopatikana katika chuo cha UDOM kwa kipindi cha miaka sita.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu hiho, Balozi Augustine Mahiga aliwataka wanafunzi waliojiunga na chuo hicho na wale wanaoendelea kutumia fursa zilizopo kujiimarisha kitaaluma na kuongeza ujuzi.

“Inawezekana vitabu havitoshi au maktaba haikidhi wingi wa wanafunzi lakini huu ni ulimwengu wa e-books mkitumia vizuri teknolijia ya google na nyinginezo ambazo walimu wenu wanazifahamu mtajikuta katika ulimwengu tofauti katika upatikanaji wa mabadiliko mbalimbali iwe ni vitabu, majarida au makala,” alisema.

Alisema chuo kinatambua changamoto zinazowakabili na kimejenga mifumo mizuri na thabiti ya kuwezesha na kukuza mawasiliano na majadiliano kati ya uongozi wa wanafunzi na menejimenti ya chuo. Alisema chuo hicho ni mahali pa kuimarisha uzalendo na umoja wa taifa kutokana na wanafunzi kuchanganyika kutoka sehemu mbalimbali za nchi.

Makamu Mkuu wa Chuo hicho Profesa Idris Kikula alisema jumla ya wahitimu katika mahafali hayo ya sita ni 4,136, wakiwa ni katika ngazi mbalimbali za cheti, stashahada, shahada ya kwanza, stashahada ya juu, shahada za uzamili na shahada za uzamivu.

Alisema kati ya hao, stashahada na cheti ni 159 na shahada ya kwanza ni 3,435 na shahada za juu ni 542. Profesa Kikula alisema idadi ya wahitimu imeongezeka kulinganisha na mwaka 2014 ambapo jumla ya wahitimu ilikuwa 3,949.

Alisema kwa upande wa shahada za juu hiyo ni idadi kubwa tangu kuanzishwa kwa chuo ambapo mwaka 2014 idadi ilikuwa 383 kati ya hao uzamivu walikuwa 14, idadi hiyo imekuwa ikiongezeka kila mwaka na kwamba tangu kuanzishwa kwa chuo idadi ya wahitimu kuanzia mahafali ya kwanza 2010 ni 26,663.

“Pia tunajivunia kuongeza nguvu kazi kwani kati ya wahitimu wa shahada ya uzamivu 20, wahitimu 15 ni walimu wa UDOM,” alisema


Related

Habari Mpya 3152637790715102438

Post a Comment

emo-but-icon

item